Wednesday 7 January 2015

MARADHI YA NGOZI YANYOTOKANA NA NGONO ISIYO SALAMA

Sunzua kitaalamu warts ni ugonjwa wa ngozi unaofahamika na wengi. Ugonjwa huu husababishwa na virusi ambavyo kitaalamu huitwa human papilloma virus.
Karibu asilimia 10 ya wanadamu wamewahi kupata athari za virusi vya ugonjwa huu, achilia mbali kuumwa sunzua.
Kwa sababu hiyo ndiyo kusema kila mtu anapaswa kufahamu ugonjwa huu kwa undani ili unapojitokeza awahi hospitali ili kuudhibiti.
Virusi vinavyosababisha ugonjwa huu huambukizwa kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine kwa njia ya ngono.
Ugonjwa huu hutokea sehemu mbalimbali za mwili, lakini huwatokea wengi sehemu za siri.
Sunzua kama ugonjwa wa zinaa, huathiri sehemu za siri pamoja na njia ya haja kubwa.
Wagonjwa ambao wanaishi na Virusi vya Ukimwi wako kwenye mazingira hatarishi zaidi ya kupata sunzua.  
Virusi vinavyosababisha maradhi ya sunzua huambukizwa kwa njia ya ngono na ni mara chache huweza kusambaa kwa njia ya kugusana.
Virusi wa maradhi haya wanajulikana kama papilloma na hujitokeza kwenye eneo la ngozi ambapo virusi hivi vimepenya. Mara nyingi hujipachika kwenye mchubuko au mpasuko wa ngozi.
Maradhi haya huweza kujitokeza kwenye ngozi kati ya miezi miwili hadi tisa baada ya kupenya kwenye ngozi.
Maradhi haya husababisha ngozi kutokuwa na muonekano wake wa kawaida.
Husababisha ngozi kuwa na milima na mabonde kiasi cha kusababisha kukatika kwa urahisi na kufanya virusi kuendelea kupenya.
Dalili za maradhi haya ni kuwa na ngozi iliyoinuka, iliyopoteza unyoofu wake na yenye muonekano mfano wa maua.
Sunzua ziko za aina tofauti kulingana na mahali ugonjwa unatokea na kuonekana kuiathiri ngozi.
Sunzua ya sehemu za siri au kwa kitaalamu condyloma acuminatum (venereal warts).
Aina hii ya ugonjwa kwa wanawake huathiri sehemu za nje za maumbile ya siri na mara nyingine huweza kujitokeza na kuathiri shingo ya kizazi.
Kwa wanaume sunzua huathiri uume wenyewe, korodani, nyonga mpaka kwenye mapaja.
Sunzua hii ya sehemu za siri kwa watu wa jinsia zote hujitokeza kama uvimbe ulioinuka au zikawa sawia bila uvimbe wa aina yoyote.
Sunzua zinaweza kuwa kubwa au ndogo, zikawa mojamoja au zikajikusanya pamoja kama mafungu zikafanana kabisa na maua.
Huwa zinaweza kutokea usoni, hasa sehemu karibu na kope ama maeneo mengine kama vile vidole vya miguu na mikono.
Sunzua huwa haziumi na sanasana huwa zinawasha na huweza kujitokeza katika kipindi cha miezi miwili mpaka tisa baada ya maambukizi ya virusi.
Kwa wanawake, sunzua ya kwenye shingo ya kizazi huweza kusababisha saratani ya shingo ya kizazi.
Kwa sababu hiyo, mwanamke anapaswa kujichunguza ili kuchukua hatua mwafaka za matibabu

No comments:

Post a Comment

.