Thursday 23 October 2014

FAIDA NA JINSI YA KUPANGA RATIBA YA CHAKULA KWA AFYA YAKO.

Ili kuwa na siha njema ni muhimu kula vizuri. Kula vizuri si rahisi, ingawa wengi wetu tunadhani kula vizuri ni kula chakula tunachokipenda – chips, kuku, mayai, nyama na vingine. Hii ni kasumba mbovu tu. Kula vizuri (au balanced diet) si lazima kula vyakula unavyopenda, bali kula vyakula vyenye afya na kujenga mwili wako. Njia moja mbadala ya kuhakikiasha unakula vizuri na kwa afya ni kuwa na ratiba ya wiki ya chakula. Leo tunaangalia umuhimu wa kupanga ratiba ya chakula kwa afya yako na familia yako.

Chakula bora (Balanced diet) ni chakula kinachokupa virutubisho vyote muhimu mwilini katika milo mitatu ya siku. Chakula bora, kama ilivyo kwa kila kitu bora, hakiliwi kwa bahati, bali huhitaji mipango madhubuti ya kupanga chakula cha kila siku kinachojali afya yako na familia.
Sasa, kuandaa ratiba ya chakula kizuri si kazi rahisi, lakini inasaidia kupunguza mawazo ya nini cha kupika na kupunguza haraka za kuandaa vyakula bila kufikiria vizuri virutubisho vinavyopatikana kwenye milo yako. Kwa kawaida ni kazi ya mama kuamua chakula gani kinaliwa nyumbani. Lakini, mie nadhani ni swala la familia nzima kuamua chakula gani kinafaa kuliwa sababu chakula ni swala la kila mtu kwenye familia. Hapa ndio panapotuleta kwenye swala zima la kupanga ratiba ya chakula kwa wiki nzima. Chakula ni kitu muhimu sana maishani, hivyo ni jukumu la kila mtu kuchangia mawazo kwenye afya ya familia, si jukumu la kumuachia mama pekee - kila mtu ana nafasi yake kwenye kutoa mchango, hata kama ni wa mawazo.
Kama uko peke yako usikate tamaa, ni rahisi zaidi maana utakuwa una uwezo wa kufanya maamuzi bila kuwa na mawazo ya kukinzana.
Swala la kuamua chakula gani kinaliwa lini ni swala la mipango na malengo. Ukifanya hivi unaweza kujijengea ratiba ya kula milo vizuri iliyojaa virutubisho unavyohitaji. Na jambo kubwa hapa ni kuokoa muda na matumizi yasiyo na tija.

Faida za ratiba ya chakula

Je ni faida gani unapata kwa kupanga ratiba ya chakula?
  • Kufahamu kirahisi vyakula vyenye afya na kwa mahitaji  yako. Mfano mzuri ni kuwa na uwezo wa kula matunda na vyakula vya protini kwa wingi
  • Ni rahisi kujua virutubisho muhimu unavyokula kwa kipindi cha wiki nzima, hivyo ni rahisi kukusaidia kutathmini afya yako kwa urahisi
  • Kuwa na chaguo zaidi ya moja ya vyakula hivyo kuzuia kula chakula aina moja kinachopendelewa na kusababisha kukosa virutubisho muhimu kwenye vyakula vingine
  • Kupanga matumizi madhubuti ya nyumbani na kuweza kuokoa fedha kwenye maswala ya chakula. Usidharau sana hii sababu chakula ndio kitu pekee kinachotumia hela nyingi kupita kiasi kwa matumizi nyumbani. Ukiweza kujua vizuri matumizi ya nyumbani utakuwa na uwezo wa kupanga matumizi yako vizuri na kufanya shughuli za maendeleo.
  • Ni njia pekee ya kuweza kujua afya yako halisi na familia yako – mfano kupunguza au kuongeza uzito
  • Ni njia mbadala ya kuwafundisha watoto wako jinsi ya kuishi vizuri na vyema wakiwa watu wazima wenye familia zao. Watoto huangalia matendo yako, siyo maneno, hivyo ni vizuri kuwaanzishia msingi mzuri wa maisha ili wapate kufaidika na maisha yako hapo baadae.
  • Kudumisha furaha nyumbani sababu kila mmoja anaona umuhimu wake katika mawazo juu ya chakula, hivyo kuwafanya watu kufurahia kujumuika kula pamoja kifamilia.

Jinsi ya kupanga ratiba ya chakula

Je unawezaje kuweka uwiano bora wa vyakula ili uweze kupata virutubisho muhimu mwilini ?
Ni vizuri kuwa na ratiba ya chakula kwa wiki nzima, hii itasaidia kujua milo ya chakula kila siku na jumla ya virutubisho unavyopata mwilini. Ratiba ya wiki inasaidia kujua ni kiasi gani cha chakula kinahitajika kwako (kama uko peke yako) au familia kwa ujumla.
Unaweza kupanga ratiba yako kama unavyopenda. Ila ni muhimu kufuata maagizo machache yafuatayo :

1. Hakikisha unapata vyakula muhimu

Angalia aina muhimu za vyakula kwa siku – matunda  na mboga za majani. Hizi ni muhimu kuwepo sababu zina virutubisho halisi vinavyohitajika mwilini. Ni vizuri kula matunda na mboga za majani zisizopungua aina 5 kwa siku. Mfano wa matunda ni ndizi, papai, nanasi, apple, chungwa n.k.

2. Kuwa mbunifu

Kula ni haki yako, lakini kwanini ule chakula aina moja wakati kuna vyakula vingi tu vitamu? Jifunze kuandaa vyakula tofauti, kula kwa rafiki, onja vyakula aina mbalimbali. Ili kuweza kutimiza hili, jaribu kula vyakula tofauti kutokana na ratiba yako. Ni muhimu kutopendelea vyakula kwenye kundi moja sababu unakosa virutubisho kutoka kwenye kundi tofauti. 
Kama kuna kitu unapendelea zaidi, weka kiwe kinapatikana mara nyingi kwenye ratiba yako. Lakini jaribu na kwengine uone ubora wake. Mfano mzuri ni kuwa mie hupendelea zaidi maharage, ni jambo zuri kula chakula nikiwa na maharage pembeni.

3. Pendelea vitu halisi

Ni rahisi sana kula vyakula visivyo na virutubisho nyumbani sababu ndio vyakula vilivyojaa kila kona ya dunia kwa sasa. Ili kuhakikisha unakuwa na afya bora, pendelea zaidi vitu halisi kuliko vile vya kuchakachua – kunywa maji badala ya juisi. Kula tunda badala ya juisi. Maji ni muhimu sana, lakini wengi tunapuuzia hii kanuni ya afya. Mfano, mtu mzima anatakiwa kunywa lita moja na nusu ya maji kwa siku. Je unazingatia hilo ?
Tunashauri uwe na ratiba ya chakula nyumbani. Ni vizuri kwa afya pia kwa kujua vizuri matumizi ya nyumbani. Mie huwa nafanya hivi kila wakati, nimeona faida zake ndio maana nakushauri na wewe. Kama umependa basi washauri na wenzio, maana kila kitu kizuri ni vyema kuwaeleza wale tuwapendao.
 KUTOKA MISOSI.COM 

No comments:

Post a Comment

.