Saturday 8 March 2014

Jinsi ya kukabiliana na ugonjwa wa kifua kikuu (TB)

Kifua kikuu (TB), ugonjwa huu husababishwa na bakteria waitwao Mycobactrium tuberculosis. Bacteria hawa (chembechembe za ugonjwa) hushambulia mapafu ya hewa. Ukikaa karibu na mgonjwa mwenye T.B. waweza kuambukizwa ugonjwa huo kwani akikohowa hutoa vijidudu hivyo vikasambaa hewani.
Kifua kikuu cha mapafu ni ugonjwa unaoambukiza kwa urahisi sana. Walio na hatari zaidi ya kuambukizwa ugonjwa huu ni wale ambao ni dhaifu, wakosefu wa lishe bora na wale wanaoishi na mtu mwenye ugonjwa huo.
Ili kukijinga na kumponyesha mgonjwa aliyekwisha upata ugonjwa huo ni lazima mgonjwa atibiwe mapema. Na hili haliwezekani mpaka dalili zake zifahamike.

Dalili za kawaida:
Kikohozi cha muda mrefu hasa mara tu baada ya kuamka; homa ndogo ndogo nyakati za mchana na kutoka jasho jingi wakati wa usiku. Kuwa na maumivu kifuani au sehemu za juu ya mgongo. Kukonda na kuwa dhaifu muda mrefu (daima) ni dalili nyingine muhimu.
Mtu akifikia hatua ya kuzidiwa dalili zifuatazo zitajitokeza. Kukohoa damu, ngozi kuwa laini na inayofifia pamoja na sauti kukwaruza. Dalili hii ya sauti kukwaruza ni mbaya sana.
Ilivyo kawaida kifua kikuu ni ugonjwa wa mapafu lakini kinaweza kutokea sehemu yoyote ya mwili ikiwemo mifupa na utumbo.. Kwa watoto wadogo kinaweza kusababisha homa ya uti wa mgongo.
Ipo pia TB ya ngozi au tezi na husababishwa na vijidudu vile vile vinavyosababisha kifua kikuu.
Kwa kawaida TB ya ngozi hukua taratibu na hudumu muda mrefu. Pia huambukiza tezi hasa zile za shingo au sehemu zile za mtulinga kati ya bega na shingo. Tezi zinazovimba hupasuka na kutoa usaha, kisha hufunga kwa muda na kupasuka tena ila kwa kawaida haziumi.
TB hii husababisha uvimbe unaoharibu uso, mabaka ya vidonda yasiyotoweka, donda ndugu au chunjua kubwa.
TB ya ngozi hutibiwa kama ile ya kifua kikuu. Ili kukomesha isirudie tena ni lazima kutumia dawa kwa muda mrefu (miezi mingi) baada yakuona hali ya ngozi imekuwa nzuri.
Mtu akihisi dalili za kifua kikuu ni lazima amuone mganga haraka ili afanyiwe uchunguzi wa ngozi, makohozi na kupiga picha (X-Ray) ya kifua.
Dawa mashuhuri kwa kutibu ugonjwa huu ni sindano ya 'Streptomisini', vidonge vya 'Para-aminosalicylici acid (P.A.S.),vidonge vya isoniacid, vidonge vya Ethambutal na Thiazetazone. Dawa hizi mara nyingi huchanganywa za aina mbili au tatu.
Kwa kawaida huchukua muda wa mwaka mmoja na zaidi hadi kupona kabisa. Hivyo ni lazima mgonjwa aendelee kutumia dawa hata kama ataona hali yake imekuwa nzuri.
Mambo yakuzingatia: Kula chakula kingi chenye wingi wa protini, vitamini na cha kukupa nguvu.
Lazima kupumzika. Acha kabisa kufanya kazi. Pumzika na lala usingizi wa kutosha.
Nyumba ikishakuwa na mgonjwa wa kifua kikuu yafuatayo yafanyike: Mgonjwa ale na kulala peke yake, ikiwezekana chumba cha peke yake. Watoto wawe mbali naye na wapewe dawa ya kinga (Vaccination). Mgonjwa anapokohoa ahakikishe kuwa anafunika kinywa chake. Mgonjwa atibiwe mara moja. Familia izidishe kula chakula bora na ifanyiwe uchunguzi wa ugonjwa huu.
Kwa mtu aliye na virusi vya ukimwi (Human Immunodeficiency Virus- HIV) yupo katika hatari zaidi ya kupata TB kwa sababu virusi vya HIV hudhoofisha nguvu na uwezo mwili kujikinga na magonjwa. 
--

No comments:

Post a Comment

.