Thursday 18 September 2014

MADHARA YA SIGARA KWA AFYA YAKO


Kuvuta sigara ni tabia ambayo imezoeleka na watu wengi ingawa ina madhara mengi Uvutaji sigara huathiri mwili kwa njia tofauti na madhara yake ni makubwa kiafya. Inakadiriwa kuwa, hadi sasa kumegunduliwa kemikali zipatazo 7,000 katika moshi wa sigara ambapo 250 kati ya hizo ni sumu na 70 zinasababisha kansa. 

Mvutaji mdogo hutumia nusu ya pakiti ya sigara kwa siku na kujikuta akiathiri mwili wake kwa kemikali hizi mara 3500 kwa mwaka. Mada na kemikali zilizo kwenye sigara huathiri karibu kila kiungo mwilini kuanzia seli hadi mfumo wa kulinda mwili.
 Kemikali zilizoko kwenye moshi wa sigara huingia katika mapafu na kuenea katika mwili mzima na kusababisha madhara makubwa kwa njia mbalimbali. Ingawa mada hizo haribifu zilizoko kwenye moshi wa sigara ni nyingi, lakini tatu ni hatari zaidi zikilinganishwa na nyingine. Mada hizo ni nikotini, carbon monoxide na tar.
 Nicotine huufikia ubongo sekunde 7 hadi 10 baada ya moshi wa sigara kuvutwa na kemikali hiyo hutapakaa katika sehemu nyingi za mwili hata katika maziwa ya mama. Nikotini ni kemikali sumu ambayo kwa muda mrefu sana inatumiwa kama dawa ya kuuwa wadudu na sumu ya panya. Inachukua nafasi ya pili kama sumu kali kabisa kutokana na athari yake mbaya kwa mwili wa binadamu.
Tar ni kemikali inayosababisha kansa mwilini inayopatikana katika tumbaku ambayo huharibu jeni muhimu zinazozuia ukuaji holela wa seli ili zisiwe za saratani. Hii ni katika hali ambayo Carbon monoxide ni gesi yenye madhara inayopatikana katika moshi wa sigara ambayo hujishikiza katika hemoglobin kwenye seli nyekundu za damu na kuzizuia zisiweze kubeba vyema oksijeni kama inavyotakiwa. Suala hilo husababisha mtu apatwe na dalili za kuwa na sumu ya gesi hiyo mwilini.
Tunapaswa kujua kuwa, kuvuta sigara huwasababishia maradhi mbalimbali wenye kuvuta sigara kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na wasiuovuta. Miongoni mwa maradhi hayo ni magonjwa ya moyo, kiharusi, kansa ya mapafu, matatizo katika mfumo wa kupumua yanayojulikana kama COPD na mengineyo. 

ONYO UVUTAJI WA SIGARA NI HATARI KWA AFYA YAKO BOFYA HAPA KULIKE PAGE NA UMUELIMISHE RAFIKI. 

No comments:

Post a Comment

.