Miezi ya hivi karibu, Makamu wa rais, Dk Mohammed Gharib Bilal alinikuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi maskini zinazoongoza kwa kuwa na wagonjwa wengi wa saratani za mfumo wa chakula na ini, ikilinganishwa na nchi zinazoendelea.



Kwa mujibu wa takwimu nchini zinaonyesha wastani wa watu 30 hadi 35 kwa kila wananchi 100,000 hufariki dunia kila mwaka kwa saratani ya mfumo wa vyakula, koo na ini. Maradhi ya saratani yanasababishwa na mambo mengi, ikiwemo ulaji wa vyakula vyenye kemikali zenye sumu. Tabia ya kufungia vyakula kwa kutumia magazeti inaweza kuchangia maradhi ya saratani. Hali hii inatokana na magazeti yaliyotumika kuwa na uchafu, kuyatumia kufungia vyakula ambavyo vipo tayari kutumika pia kunaweza kusababisha mtu kupata matatizo ya tumbo.

Wino wa kuchapa magazeti unatengenezwa kwa kutumia mchanganyiko wa vitu mbalimbali ikiwemo mafuta ya petrol.

Kemikali nyingine pia hutumika ili kufanya wino uingie katika karatasi wakati wa uchapaji. Kemikali hizo zina vitu vinavyoweza kusababihsa saratani na kuathiri mfumo wa uzazi hivyo kuufanya usitende kazi zake kikamilifu. Kutumia vyakula vilivyochanganyika na kemikali hizi kunasababisha watu kuathirika.

Katika miaka ya 90, mafuta yanayotokana na soya yalikuwa yanatumia kutengeneza wino uliotumika kuchapa magazeti. Chanzo hiki ni rafiki wa mazingira na siyo sumu.

Hata hivyo, kukua kwa teknolojia kumefanya yawapo amtumizi ya kisasa ziaidi yanayotokana na kemikali ambazo ni hatari kwa afya ya binadamu kama vile mafuta ya petroli.

Wino unaotokana na soya au maji una kiwango kidogo cha kemikali hizo hatari zinazoweza kusababisha mlipuko zinapokutana na moto. Matumizi ya magazeti kufungia vyakula ni tabia ya kila siku kwa watanzania wengi na watu wengine duniani.

Hata hivyo, tabia hiyo ni ya hatari kiafya, watu wakitumia amgazeti kufunga vyakula hasa vile vilivyokaangwa kwa mafuta na huku yale mafuta bado hayajakauka. Mafuta hayo yanayonywa wino kutoka katika magazeti na kuingiza katika vyakula.

Vyakula vinavyokaangwa na kufungwa kawa kutumia magazeti chini ni pamoja na chips, samaki, kuku, nyama, chapatti, maandazi, ndizi, mihogo na mayai.

Baadhi ya wafanyabiashara wa vyakula vya kukaanga wanatumia magazeti kukausha mafuta. Kitendo hiki nacho ni hatari sana kwa sababu wino utanyonywa na kuingizwa katika vyakula.

Watu wengine wanatumia magazeti na kufunga mboga za majani na kuziweka katika frii wakiamini kuwa mboga hizo zitakaa kwa muda mrefu bila ya kubadilika. Kitendo hiki nacho ni hatari kwa sababu wino unaweza kuingia katika mboga hizo.

Tukiangalia zaidi takwimu za kiwango cha ugonjwa wa saratani za aina zote, tangu mwaka 1960 mpaka 1980, idadi ilikuwa ndogo. Lakini kuanzia mwaka 1990 mpaka 2005 iliongezeka sana.